Thursday 16 March 2017

Kesi ya Mwenyekiti wa Yanga Yusuf Manji kusikilizwa tena leo.|Soma

Kesi inayomhusu Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji ya juu ya matumizi ya dawa za kulevya aina ya Heroine, inatarajiwa kusikilizwa tena leo Alhamisi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya kuahirishwa kwa mara ya mwisho Februari 16, mwaka huu.

Manji anatuhumiwa kutumia madawa hayo kinyume na sheria ya mwaka 2015 ya kuzuia na kupambana na madawa ya kulevya kifungu cha 17 (1) namba 5 ambapo inadaiwa Manji alitumia dawa hizo Februari 6 na 9, mwaka huu.

Kesi hiyo inasikilizwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Cyprian Mkeha huku upande wa Jamhuri ukiwakilishwa na Wakili Osward Tibaloyekomya huku upande wa Manji ukiongozwa na Wakili Alex Mgongolwa.

Baada ya kusikilizwa kwa mara ya kwanza kwa kesi hiyo, Manji alikataa mashtaka hayo na kuachiwa nje kwa dhamana ya milioni 10 iliyotolewa na Katibu wa Yanga, Charles Mkwasa.

Lakini kuna uwezekano mkubwa wa kusikilizwa kwa kesi hiyo bila ya Manji kuwepo kutokana na kuumwa kwani kwa sasa amelazwa kwenye Hospitali ya Aga Khan ambapo anasumbuliwa na tatizo la moyo.

0 comments:

Copyright © 2017 KwilasaNewsline | We Call Away| All Right Reserved|
Scroll To Top