Monday 6 March 2017

Kauli ya Rais Dkt. John Magufuli kuhusu watanzania waliofukuzwa Msumbiji.|Soma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli jana tarehe 05 Machi, 2017 amemaliza ziara yake ya kikazi ya siku 4 katika mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara.

 

Kabla ya kuondoka Mjini Mtwara na kurejea Jijini Dar es Salaam Mhe. Rais Magufuli alifanya mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Mashujaa Mjini Mtwara ambapo alisema Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kuhakikisha inasukuma maendeleo ya Mtwara na Lindi kwa nguvu kubwa kwa manufaa ya wananchi. 

 

Alisema Serikali imedhamiria kutilia mkazo juhudi za uendelezaji wa bandari ya Mtwara, ujenzi wa barabara, uimarishaji wa miundombinu ya nishati ya umeme, ujenzi wa viwanda vikubwa na usimamizi mzuri wa shughuli za kilimo ambavyo vitasaidia kukuza uchumi, kuzalisha ajira na kuboresha maisha ya watu. 

 

Mhe. Rais Magufuli aliwapongeza viongozi na wananchi wa Mkoa wa Mtwara kwa mafanikio yaliyopatikana katika soko la korosho lililopita na ameagiza wale wote waliohusika kufuja fedha za wakulima wachukuliwe hatua. 

 

Aidha, Mhe. Dkt. Magufuli alisema Tanzania itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake mzuri na nchi jirani ya Msumbiji na ametaka suala la wahamiaji haramu wanaoondolewa nchini humo wakiwemo Watanzania lisikuzwe huku akisisitiza kuwa Serikali haiwezi kuwatetea watu wanaoishi katika nchi nyingine bila kufuata sheria. 

 

Kuhusu Mkoa wa Mtwara kufanya vibaya kielimu, Mhe. Rais Magufuli amewataka wananchi wa Mtwara kubadilika kwani juhudi za Serikali kuwapelekea maendeleo hazitakuwa na maana kama wananchi watakuwa hawana elimu. 

 

“Nimeambiwa hapa watu wanapenda sana disco na ngoma, watoto badala ya kusoma wanacheza disco, hapo tunakwenda pabaya” alisisitiza Mhe. Rais Magufuli. 

 

Mkutano wa Mhe. Rais Magufuli Mjini Mtwara ulidhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi, Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Fedha na Mipango Dr. Philip Mpango, Wabunge na viongozi wa taasisi. 

 

Gerson Msigwa 

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

0 comments:

Copyright © 2017 KwilasaNewsline | We Call Away| All Right Reserved|
Scroll To Top