Maalim Seif |
Bodi ya Wadhamini ya Chama cha Wananchi (CUF ), imefungua kesi ya madai dhidi ya wanachama wake nane akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Magdalena Sakaya.
Kesi hiyo imefunguliwa (Jana) katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ikitaka wanachama hao wasijihusishe na harakati zozote za chama hicho.
Mbali ya Sakaya ambaye pia ni mbunge wa Kaliua mkoani Tabora, wadaiwa wengine ni Thomas Malima, mbunge wa Mtwara Mjini,Mafta Nachumu, Omar Mhina Masoud, Abdul Kambaya, Salama Masoud, Zainabu Mndolwa na Jafari Mneke.
Maombi hayo mbayo yametajwa mbele ya Hakimu Mkazi, Wilbard Mashauri yamewasilishwa na Wakili wa bodi, Hashim Mziray na yamepangwa kusikilizwa kesho.
Katika maombi hayo yaliyopewa namba 1 ya mwaka 2017, bodi inaiomba mahakama kutoa zuio kwa wadaiwa kutojihusisha katika masuala yeyote yanayohusiana na chama hicho.
Mbali ya maombi hayo, pia Wakili Mziray amewasilisha maombi madogo ya kuiomba mahakama kuwaamuru wadaiwa wasijihusishe na mikutano ya chama hicho.
Aidha, Mziray aliomba maombi yao madogo yasikilizwe kwa upande mmoja wa wadai tu kwa kuwa wamechelewa kuwapatia nyaraka za madai yao wadaiwa.
"Mheshimiwa tunaomba tusikilizwe upande mmoja ukizingatia maombi yameletwa chini ya hati ya dharula na kwa mujibu wa sheria mahakama hii... inayo mamlaka ya kufanya hivyo".
0 comments:
Post a Comment