Thursday 20 April 2017

Rais Magufuli amewataka Wafanyakazi Nchini kuchapa kazi na kuwahakikishia kuwa Serikali itawalinda.|Soma

Rais wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 20 Aprili, 2017 amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) na kuwahakikishia kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza na kuimarisha zaidi ushirikiano kati yake na wafanyakazi kwa manufaa ya Taifa.

Katika Mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, Mheshimiwa Rais Magufuli amesema pamoja na kuimarisha ushirikiano huo, Serikali ipo tayari kupokea maoni na ushauri wowote utakaotolewa na vyama vya wafanyakazi wenye lengo la kuboresha maslahi ya wafanyakazi na kuongeza tija kazini.

Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali inatambua changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi na itaendelea kuchukua hatua za kukabiliana nazo kama ambavyo imeanza kufanya hivyo.

“Nataka kuwahakikishia nyinyi viongozi wa TUCTA na wafanyakazi wote kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inawapenda wafanyakazi na ipo tayari kuwapigania, jambo la msingi tutangulize maslahi ya Taifa, kawaambieni wafanyakazi wachape kazi na Serikali itawalinda” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Kwa upande wao Viongozi wa TUCTA wakiongozwa na Rais wa Shirikisho hilo Bw. Tumaini Nyamhokya wamempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali yake kujenga uchumi imara, kuimarisha utendaji kazi wa watumishi wa Serikali, kupambana na rushwa, kuondoa watumishi hewa na kulipa madeni ya watumishi.

Viongozi hao wameahidi kushirikiana na Serikali katika kusimamia haki na wajibu wa wafanyakazi na wameomba Serikali iendelee kufanyia kazi masuala mbalimbali ya wafanyakazi ikiwemo kuwalipa stahili zao na kuboresha mazingira ya kazi.

0 comments:

Copyright © 2017 KwilasaNewsline | We Call Away| All Right Reserved|
Scroll To Top